Ads

Simba inahitaji wanaume watatu wa nguvu...


Review..

Image result for simba sc

Simba itakuwa inasafiri labda kwenda Rwanda, Yanga itakuwa inasafiri kwenda Misri. Kule kwa Yanga kiasi wametimia, huku kwa Simba kunahitajika wanaume watatu wengine kabla ya kupanda ndege kwenda hiyo safari yao.
Simba inahitaji kuingia sokoni kwa umakini na kununua wachezaji watatu wa kigeni wa maana ambao, kwa hapa nchini sijawaona mpaka sasa. Mgongo wa timu ni mlinzi wa kati kiongozi mwenye uzoefu.
Kisha kiungo mahiri mwenye nguvu na uzoefu, halafu mshambuliaji wa nguvu anayeweza kufunga mabao 20 ya msimu.
Kwa kuanzia katika ushambuliaji Simba wamekwenda kwa John Bocco. Siyo mbaya. Kwa kulinganisha washambuliaji ambao wanao sasa hivi, Bocco ni bora zaidi. Bocco aliye fiti bila ya majeraha ni bora kuliko Laudit Mavugo au shujaa wa juzi, Fredric Blagnon.
Anahitajika mtu kama Donald Ngoma wa Yanga. Mtu msumbufu, mwenye nguvu, asiyeogopa, lakini cha msingi zaidi awe na jicho la kuona lango. Niliandika mitandaoni, Ngoma hajaichezea Yanga katika Ligi tangu Januari, lakini Mavugo hakuweza kufikia mabao yake katika ligi.
Kwa muda mrefu Simba imekosa mshambuliaji tishio huku ikishindwa kufanya vyema katika soko la uhamisho la wachezaji wa kimataifa. Tangu alipoachwa huru Amiss Tambwe na kununua Dan Sserunkuma, Simba haijapata mtu wa uhakika pale mbele.
Katika nafasi ya ulinzi Simba wanahitaji mtu kiongozi, mbabe, mwenye akili ya mpira kama Serge Paschal Wawa. Huyu Method Mwanjali inaonekana umri umesogea na ndiyo maana hata majeraha yake yamechukua muda mrefu.
Hata kama angekuwa fiti, katika mechi za kimataifa Simba tayari ilikuwa inahitaji beki wa nguvu wa kucheza naye sambamba. Juzi James Kotei amecheza vizuri katika nafasi hiyo, lakini nadhani bado anahitajika mlinzi wa nguvu zaidi.
Simba pia wanahitaji kiungo mwingine mwenye mamlaka uwanjani. Kiungo ambaye pia atakuwa kama kiongozi wa eneo hilo. Kuna utoto mwingi katika eneo la kiungo la Simba hasa katika kutengeneza mashambulizi ya haraka haraka.
Anahitajika kiungo wa aina ya Athuman Idd Chuji au Patrick Mafisango. Kiungo mwenye mamlaka dhidi ya wenzake na wachezaji wa timu pinzani.
Anayeweza kucheza pasi ndefu na fupi pale inapolazimu. Anayeweza kubadili uwanjani na kuacha soka la kitoto ambalo baadhi ya viungo wa Simba wanacheza kwa sasa.
Kwa kuanzia Simba wanahitaji kuwa na wanaume watatu wa nguvu katika idara hizo tatu ambazo ni muhimu zaidi. Wakati mwingine timu zetu zinajaza wachezaji bila ya umakini mkubwa. Jaribu kuona utoto ambao Simba waliufanya katika dirisha dogo la uhamisho. Wachezaji waliowachukua walijaza idadi zaidi badala ya kujaza ubora katika kikosi.
Simba wakileta mzaha huu katika mechi za kimataifa hawatafika mbali ingawa ni tamaduni yao kucheza vema katika mechi za aina hiyo.
Maeneo mengine wanaweza kujaza wachezaji mahiri wa nyumbani, lakini hili la mlinzi wa kati, kiungo wa kati na mshambuliaji mahiri wa kati halihitaji mzaha.
Nimejaribu kuangalia wachezaji wetu wengi wazawa katika nafasi hiyo naona bado hawapo tayari. Itazame vizuri Yanga. Ilibadilika zaidi pale walipowachukua Thaban Kamusoko na Ngoma. Mmoja aliibadili timu katika eneo la kiungo mwingine akaibadili katika eneo la ushambuliaji. Tambwe na Obrey Chirwa lilikuwa ongezeko la ubora tu, lakini tayari walishakuwa na msingi wa timu.
Azam ilibadilika zaidi wakati walipowaleta pacha, Kipre Tchetche na Kipre Balou. Mmoja akaibadili safu ya kiungo na mwingine akaibadili safu ya ushambuliaji. Kina John Bocco na Himid Mao walikuwa ongezeko tu la ubora wao. Wameondoka hao wawili timu imeyumba. Simba wasijidanganye kabisa. Timu yao bado ina mapungufu na haipo tayari sana kwa mechi za kimataifa ingawa tayari ina tiketi mkononi. Wasifanye makosa ambayo wameyafanya katika dirisha kubwa lililopita halafu wakayarudia tena katika dirisha dogo.
Hawa wanaume watatu wa kuibadili timu wasiwe wachezaji wa bei rahisi wala wale wa kuja kufanyiwa majaribio. Mchezaji mzuri hafanyiwi majaribio.
Ni kama ambavyo akina Kipre na Ngoma hawakufanyiwa majaribio. Mchezaji mzuri anajulikana na hawezi kukubali kufanyiwa majaribio. Wakishapata wachezaji wa nguvu katika nafasi hizo tatu nadhani tunaweza kukutana Uwanja wa Ndege kwa furaha bila ya wasiwasi. Kwa hali ilivyo sasa, kama wanasumbuliwa na Kagera Sugar, Toto na Mbao basi wasitegemee maajabu katika mechi za kimataifa. Watakuwa wanamaliza nauli tu. Kwa sasa kuna wavulana wengi katika kikosi chao.
Hawawezi kucheza mechi ngumu na hawawezi kubadili matokeo kirahisi.
Hata wakati huu wakiwa wanawania pointi za mezani Fifa kitu cha msingi zaidi kwao ilikuwa kutafakari namna ambavyo pengo la pointi nane baina yao na Yanga lilivyopotea wakati Ligi ikiendelea
Ilitokana na kuwa na wavulana wengi mabishoo ndani ya uwanja ambao, hawakujua kuzicheza mechi ngumu, sasa itakuwaje zile za kimataifa?
Source, Edo ku mwembe

No comments

Theme images by andynwt. Powered by Blogger.