Ads

Samata afunguka wakati stars ikielekea Cameroon...

Image result for samata


KOCHA Mkuu wa timu soka yaTaifa, Taifa Stars, Salum Mayanga amejigamba kuifunga Lesotho leo katika mechi ya kutafuta kufuzu fainali za michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (Afcon) 2019.

Mechi hiyo ya kukata na shoka inatarajiwa kuchezwa saa 2 usiku katika uwanja wa Azam, Chamazi, Jijini Dar es Salaam. Mayanga alisema jana, wamefanya maandalizi ya kutosha kwa ajili ya mchezo huo hivyo wana matumaini makubwa ya kushinda.

Alisema miezi miwili iliyopita walicheza michezo miwili ya kirafiki na walipiga kambi ya ndani na nje nchini Misri. “Tunacheza na timu nzuri ambayo msimu uliopita ilionesha kiwango kizuri katika mashindano haya. Pia nimeangalia mechi ambazo wamecheza nyuma na kugundua udhaifu wao upo wapi,” alisema Mayanga.

Nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta alisema timu ipo vizuri na wachezaji wamejiandaa vizuri kushinda. Kocha wa Lesotho, Moses Malieho alisema nao wamejiandaa vizuri kwa sababu wanafahamu Tanzania siyo timu rahisi.

Alisema amefuatilia michezo ya Taifa Stars ya nyuma waliyocheza na Nigeria na Botswana na kubaini maeneo yenye upungufu atakaoutumia ili kuwashinda. “Tulijiandaa kwa kucheza mchezo wa kirafiki dhidi ya Msumbiji na kushinda 1-0 lakini tumekuja kupambana kwani Tanzania si timu ya kubeza,” alisema.

Viingilio vya mchezo huo vimepangwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuwa Sh 5,000 viti vya kawaida na Sh10,000 VIP. Katika michuano hii ya AFCON, Tanzania iko kundi L na Lesotho, Uganda na Cape Verde. Timu itakayoongoza kundi ndiyo itafuzu kwa fainali za 2019 Cameroon.

No comments

Theme images by andynwt. Powered by Blogger.